UN YAICHUNGUZA TANZANIA JUU YA UHUSIANO WA BIASHARA YA MAKOMBORA YA KIVITA NA KOREA KASKAZINI.

Tanzania na Uganda ni kati ya nchi kadhaa za Afrika zinazochunguzwa kwa kukiuka vikwazo vilivyowekwa dhidi ya Korea Kaskazini, Jopo la wataalam wa Umoja wa Mataifa limesema.
Ripoti ya Septemba 9 ilitolewa siku mbili kabla ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa pamoja kuweka vikwazo vipya vinavyo ishinikiza Korea Kaskazini kufanya mazungumzo juu ya silaha zake za nyuklia.
Jopo la watu wanane limesema linafanya tathmini juu ya taarifa kutoka kwa vyanzo vya habari vya nchi wanachama wa UN ambavyo havijatajwa majina vikisema kuwa Tanzania iliingia mikataba ya kijeshi na Korea Kaskazini yenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 12.5.
Kampuni ya Haegeumgang Trading Corporation inasemekana kuwa inafanya ukarabati na kurekebisha mifumo ya makombora ya kivita na ulinzi wa anga kuifanya iwe ya kisasa.
“Serikali ya Tanzania mpaka sasa bado haijatoa maelezo kujibu mambo ambayo yamedadisiwa na jopo hilo,” wachunguzi wa UN wamesema.
Jopo hilo limeongeza kuwa limeendelea kufanya uchunguzi wake juu ya Korea Kaskazini kutoa mafunzo ya kijeshi kwa jeshi la Uganda na vikosi vya polisi nchini humo, “hususan Jeshi la Anga la Uganda.”
Pia uchunguzi huo umejikita katika shughuli zinazofanywa na mwakilishi wa kampuni ya uchimbaji madini ya Korea Mining Development Trading Corporation ambaye alisafiri kwenda Uganda akitokea Syria.
Pia jopo hilo limeongeza kusema kuwa linafuatilia kazi ya mwambata wa kijeshi katika ofisi ya ubalozi wa Korea Kaskazini nchini Kampala.
“Uganda bado haijajibu maswali yaliyoulizwa na jopo hilo,” ripoti hiyo imesema.

Maoni