HALI YA UCHUMI NI MBAYA SERIKALI INATAKIWA KUKOPA PESA ILI KULIPA MISHAHARA.

 Mbunge wa Kigoma Mjini na Kiongozi  ACT- Wazalendo, Zitto Kabwe amefunguka na kutoa sababu kwanini mapato ya serikali yameshuka na kusema serikali inapaswa kutazama upya utendaji wake vinginevyo itabidi ikope ili kulipa mishahara kwa watumishi.

Zitto Kabwe amesema kuwa kwa miezi ya Julai na Agosti mwaka huu mapato ya serikali yalishuka mpaka shilingi 600 bilioni na kusema ni maporomoko makubwa hivyo madhara yake ni makubwa. 
"Ni mporomoko mkubwa Sana na sio jambo la kushangilia hata kidogo. Madhara ya kushuka kwa mapato ni makubwa kwani mishahara ya watumishi wa Umma peke yake ni Shilingi 570 bilioni Kwa mwezi" alisema Zitto Kabwe
Aidha kiongozi huyo ameelezea sababu kubwa iliyopelekea mapato ya nchi kushuka  
"Mzee Harry Kitilya alipata kuniambia mwaka 2013 " Mwenyekiti, TRA inatoza kodi kutoka kwenye shughuli za biashara zinazozalisha mapato na sio kutoka kwenye biashara tu ". Kitilya alikuwa na maana kuwa kama hakuna shughuli za biashara ( business transactions), huwezi kutoza kodi. Maelezo haya yanaeleza kwanini mapato ya serikali yameshuka. Shughuli za biashara zimeshuka sana nchini na hivyo kupelekea kuporomoka Kwa mapato" alisema Zitto Kabwe
Zitto Kabwe aliendelea kutoa ufafanuzi juu ya jambo hili la kuporomoka kwa mapato ya serikali 
"Kodi inayoingiza mapato mengi Serikalini ni PAYE ( kutoka mishahara ya wafanyakazi). Kitabu cha mapato ya serikali kuu cha mwaka 2016/17 kinaonyesha kuwa wafanyakazi wote wa sekta ya Umma na sekta binafsi walichangia jumla ya shilingi trilioni 3 kwenye mapato yote ya Serikali. Hivi karibuni tumeshuhudia makampuni yakipunguza wafanyakazi na mengine kufungwa. Pia Serikali yenyewe ilipunguza watumishi iliyowaita hewa na wenye vyeti feki. Hivyo eneo kubwa la kodi ya PAYE limeathirika" alisisitiza Zitto Kabwe 
Mbali na hilo Zitto Kabwe aliitaka serikali kutazama upya utendaji wake ili kuweka mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji nchini na kudai kama serikali haiatafanya hivyo itafika mahali itabidi ikope pesa ili kulipa mishahara ya watumishi mbalimbali. 
Source East Radio
 

Maoni